Unordered List


Blogger Tips and TricksLatest Tips And TricksBlogger Tricks

Tuesday, 21 April 2015

Maandamano makubwa ya wananchi wa Bahrain dhidi ya utawala wa Aal Khalifa

Sambamba na kukaribia siku ya kusikilizwa kesi ya Sheikh Ali Salman, Katibu Mkuu wa harakati ya Kiislamu ya Al Wifaq, wananchi wa Bahrain wamefanya maandamano makubwa katika mji mkuu wa nchi hiyo Manama wakitaka kiongozi huyo pamoja na wafungwa wengine wote wa kisiasa waachiwe huru na kukomeshwa vitendo vya ukatili na ukandamizaji vya utawala wa Aal Khalifa dhidi ya raia. Sheikh Ali Salman, ambaye ni mmoja wa maulamaa mashuhuri wa Bahrain na Katibu Mkuu wa harakati muhimu zaidi ya kisiasa ya nchi hiyo alitiwa nguvuni na vikosi vya utawala wa Aal Khalifa mwishoni mwa mwaka jana.
 Kwa upande mwengine wananchi wa Bahrain siku ya Jumamosi, ambayo imo kwenye masiku ya mnasaba wa kukumbuka tukio la kubomolewa makumi ya misikiti na vikosi vya utawala wa Aal Khalifa, walisali Sala za Adhuhuri na Alasiri kwenye magofu ya msikiti wa Ainun Rastan kwenye eneo la Aali, katika mji mkuu Manama. Waumini walioshiriki kwenye Sala hizo za jamaa waliutaka utawala wa Aal Khalifa uache kuhujumu na kukandamiza uhuru wa kuabudu. Wananchi wa Bahrain walisali Sala za jamaa za Magharibi na Isha pia katika magofu ya msikiti wa Al Alawiyyat uliokuwa kwenye eneo la Az Zanj, ambao pamoja na misikiti mingine 37 ulibomolewa na kusawazishwa na ardhi katika ubomoaji misikiti uliofanywa na utawala wa Aal Khalifa mnamo mwaka 2011. Inafaa kuashiria hapa kuwa hakuna aina yoyote ya jinai na ukatili ambao haujafanywa na utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa katika kuwakandamiza wananchi wa Bahrain. Kuanzia mauaji na kuwatia korokoroni wanaharakati wa kisiasa, mpaka kuharibu na kubomoa majengo ya kidini na ya ibada ni jumla ya jinai na ukandamizaji unaofanywa na utawala wa kiimla wa Aal Khalifa. Ilikuwa ni kutokana na siasa hizo za kidikteta na ukandamizaji ndipo mnamo mwezi Februari mwaka 2011, wananchi wa Bahrain walianzisha harakati dhidi ya utawala wa Mfalme Hamad bin Issa Aal Khalifa ya kudai mageuzi ya kisiasa, kiuchumi na kijamii. Lakini jibu la utawala huo ambao umekuwa ukisaidiwa na askari wa vikosi vya kigeni hususan wa Saudi Arabia ni kushadidisha ukandamizaji pamoja na kuwatia nguvuni na kuwatesa wapinzani. Matokeo ya sera hizo za ukandamizaji za utawala wa Aal Khalifa katika kipindi cha miaka minne hadi sasa ni kushuhudiwa maelfu ya wafungwa wa kisiasa kwenye jela za nchi hiyo. Kwa mujibu wa duru za habari, kuna wafungwa wa kisiasa wapatao elfu kumi nchini Bahrain ambao kutokana na idadi ya raia wote wa nchi hiyo, wameufanya utawala wa Aal Khalifa kuwa moja ya tawala zenye wafungwa wengi zaidi wa kisiasa waliofurika kwenye magereza yake. Vitendo vya utawala wa Aal Khalifa vinadhihirisha jinsi utawala huo usivyoheshimu si uhuru wa kisiasa tu wa wananchi wa Bahrain, bali unavyowanyima pia wananchi hao haki zao nyengine za msingi ikiwemo ya kuabudu na kufanya shughuli zao za kidini kwa uhuru. Msingi wa siasa za utawala wa Aal Khalifa ni kushadidisha vitendo vya kuvunjia heshima matukufu ya kidini ya wananchi hususan Waislamu wa Kishia ambao ndio wanaounda idadi kubwa zaidi ya raia wa Bahrain. Kutokana na dhana potofu uliyonayo, utawala wa Manama unadhani kwamba kwa kubomoa misikiti na kuvunjia heshima matukufu ya kidini ya wananchi utaweza kuwafanya wananchi hao waghairi kuendeleza mapambano yao dhidi ya mfumo wa kifalme unaoitawala Bahrain. Matukio yanayojiri Bahrain yanadhihirisha wazi kwamba hatua za utawala wa Aal Khalifa za kupiga vita dini na kuwanyima raia haki zao sio tu hazijaweza kuiyumbisha hata chembe harakati ya wananchi hao, bali badala yake zimezidi kufichua na kuweka wazi zaidi mbele ya fikra za waliowengi sura halisi ya kidikteta ya watawala wa Bahrain na kukoleza zaidi moto wa upinzani wa wananchi dhidi ya utawala huo…/ 

No comments:

Post a Comment