Unordered List


Blogger Tips and TricksLatest Tips And TricksBlogger Tricks

Friday, 12 December 2014

Umoja wa Mataifa: Mapambano dhidi ya waasi yatachukua muda mrefu mashariki mwa DRC

Umoja wa Mataifa ulitangaza jana kuwa, mapambano dhidi ya makundi ya wanamgambo waasi na yale yanayosababisha ghasia na machafuko yatachukua muda mrefu huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Hivi sasa, viongozi wa serikali ya Kongo pamoja na wale wa Umoja wa Mataifa wanalinyooshea  kidole cha lawama kundi la waasi wa ADF NALU wa nchini Uganda kwa kusababisha ukosefu wa amani na utulivu nchini Kongo. Hayo yanajiri katika hali ambayo, Martin Kobler, Mkuu wa Operesheni za kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini Kongo MONUSCO hajatangaza kinagaubaga kama kundi la ADF NALU limehusika na machafuko yanayoendelea mashariki mwa nchi hiyo. Imeelezwa kuwa, waathiriwa wa mashambulio ya waasi yaliyoanza mwezi Oktoba hadi sasa katika mji wa Beni ulioko katika jimbo la Kivu Kaskazini, mashariki mwa Kongo imefikia watu 250. Waasi wa ADF wamejikita mashariki mwa Kongo tokea mwaka 1995. Baadhi ya ripoti zinaeleza kuwa kundi hilo la waasi wa Uganda lilihusika na mauaji ya watu wasiopungua 13 yaliyofanywa siku za Jumamosi na Jumapili iliyopita huko mashariki mwa Kongo. Kabla ya hapo, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio lililopendekezwa na Ufaransa na Uingereza la kuitaka serikali ya Kongo iwatimue waasi walioko mashariki mwa nchi hiyo. Kuhusiana na kadhia hiyo, wanachama wa kudumu na wasio wa kudumu wa baraza hilo walitoa taarifa ya kuunga mkono kuwepo hali ya utulivu na amani nchini humo, na kusisitiza suala la  kupokonywa silaha waasi hao. Hata hivyo, ADF NALU sio kundi pekee la waasi linalosababisha ukosefu wa amani na utulivu katika eneo la mashariki mwa Kongo, kwani licha ya waasi hao wa Uganda, kundi jingine la waasi wa Kihutu la Democratic Forces for the Liberation of Rwanda 'FDLR' la nchini Rwanda linalovuruga amani na utulivu nchini Kongo. Makundi hayo yamekuwa yakiwatumia watoto kwenye medani za vita na hata kuwadhalilisha kijinsia watoto na wanawake katika nchi hiyo.  Wahutu wa Rwanda walikimbilia  nchini Kongo  kwenye muongo wa 1990  na kuunda kundi la waasi, na imeelezwa kuwa, idadi kubwa ya wanamgambo wa kundi hilo ni watu waliohusika na mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 nchini Rwanda. Hii ni katika hali ambayo, wataalamu wengi wanaamini kwamba, propaganda kubwa zinazofanywa na madola ya Magharibi kuwa zinashirikiana na Kongo kwa lengo la kurejesha amani na utulivu nchini humo,  ni mchezo wa kisiasa tu na wala nchi hizo hazina azma  thabiti ya kurejesha amani katika eneo la mashariki mwa Kongo. Kwa hakika viongozi wa Magharibi, wao wenyewe ndiyo wasababishaji wakuu wa  machafuko na mapigano barani Afrika na hasa nchini Kongo ili waweze kuendelea kubaki kijeshi kwenye maeneo mbalimbali na kupora maliasili na utajiri wa nchi hizo. Wadadisi wa mambo wanaeleza kuwa, mashirika ya kigeni yakiwa na lengo la kupora maliasili na utajiri wa Kongo, yanataka machafuko na mapigano yaendelee nchini humo. Nazo nchi za eneo la Maziwa Makuu ya Afrika zinajaribu kulinda maslahi yao kwa kuendelea machafuko mashariki mwa Kongo. Kabla ya hapo, Umoja wa Mataifa uliunda jopo la wataalamu la kuchunguza mgogoro wa Kongo, na kutoa ripoti iliyokuwa ikizituhumu nchi za Rwanda na Uganda kuwa zinawapatia silaha waasi, kuwachochea wanajeshi wa serikali ya Kinshasa watoroke jeshini pamoja na kuwapatia waasi hao msaada wa kiintelijinsia. Katika hali kama hiyo, hatua ya Umoja wa Mataifa ya kutangaza kuendelea mapigano na mapambano dhidi ya makundi ya waasi mashariki mwa Kongo, inaweza kuwa ni tahadhari na indhari ya kukaririwa majanga ya kibinadamu  katika eneo hilo.

No comments:

Post a Comment