Unordered List


Blogger Tips and TricksLatest Tips And TricksBlogger Tricks

Friday, 19 December 2014

Marekani ilitaka kushambulia vinu vya nyuklia China

Nyaraka za siri zilizokuwa zimefichwa kwenye masjala ya Wakala wa Usalama wa Taifa wa Marekani NSA zinaonyesha kuwa, Marekani ilikuwa na mpango wa kushambulia kwa makombora vinu na mitambo ya nyuklia ya China. Taarifa zinasema kuwa, Marekani ilichukua uamuzi wa kuvishambulia kwa makombora vinu na mitambo ya nyuklia ya China wakati wa tawala za marais John F Kennedy na Lyndon B. Johnson katika muongo wa sitini. Nyaraka hizo za siri zinaonyesha kuwa, aliyekuwa Mkuu wa Kamisheni ya Nyuklia ya Marekani kuanzia mwaka 1961 hadi 1971 alithibitisha juu ya kutaka kufanyika shambulio hilo dhidi ya mitambo ya nyuklia ya China. Mkuu huyo alieleza kwenye nyaraka hizo kwamba uamuzi huo wa Marekani ulichukuliwa baada ya China kukataa kujiunga kwenye makubaliano ya upigaji marufuku majaribio ya silaha za nyuklia. Taarifa hizo zinaeleza kuwa, Umoja wa Kisovieti wa Urusi ya zamani pia ulikubali kushirikiana na Marekani kwa ajili ya kuvishambulia vinu vya nyuklia vya China. Hata hivyo, Marekani ilishindwa kutekeleza azma yake hiyo kwa hofu kwamba China ingelitoa radiamali kali dhidi ya Taiwan, inayohesabiwa kuwa mshirika mkubwa wa Marekani katika eneo la Mashariki ya Mbali.

UN yatafuta milioni 810 kuwasaidia wakimbizi S/Kusini

Mashirika ya Kimataifa ya Kutoa Misaada ya Kibinadamu yanatafuta dola milioni 810 kwa ajili ya kuwasaidia wakimbizi wa Sudan Kusini ifikapo mwakani. Mkuu wa Shirika la Kuwahudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR ametahadharisha kwamba, iwapo mapigano hayatasimamishwa nchini Sudan Kusini na kufikiwa makubaliano ya amani, kuna uwezekano mkubwa wa kuongezeka idadi ya wakimbizi wa nchi hiyo kwenye kambi za wakimbizi zilizoko nchi jirani na kufikia idadi ya wakimbizi laki nane na elfu ishirini na moja. Mkuu wa Shirika la Kuwahudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR amezitaka nchi jirani na Sudan Kusini kushirikiana na shirika hilo la kimataifa kwa lengo la kuhifadhiwa usalama na maisha ya wakimbizi walioko kambini. Taarifa zinasema kuwa, wakimbizi wasiopungua elfu tisini na saba wanakabiliwa na hali mbaya kwenye kambi za Umoja wa Mataifa zilizoko nchini Sudan Kusini 'UNMISS'. Wakati huohuo, Amina Mohamed Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Biashara ya Kimataifa wa Kenya amewataka wafadhili wa kimataifa kutoa misaada yao ya kifedha kwa ajili ya kuzuia kujitokeza mgogoro wa kibinadamu nchini humo. Waziri Amina Mohamed amesisitizia udharura wa kukomeshwa mapigano na kurejeshwa amani na utulivu nchini Sudan Kusini.

Mh Zitto Kabwe ausishwa na ulaji wa Escrow | BUNGE matargide

Matokeo ya uchaguzi TZ yaonesha kuimarika upinzani

Matokeo ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika juzi nchini Tanzania yanaonyesha kuimarika upinzani nchini humo baada ya kupata viti vingi vya uenyekiti wa mitaa na vijiji, pamoja na mamia ya wajumbe wa Serikali hizo.
Hayo yanaonyesha kuwa vyama hivyo vimeanza kuimarika katika ngazi za chini, tofauti na ilivyokuwa mwaka 2009, katika uchaguzi ambao CCM kilipata ushindi wa kishindo wa asilimia 91.72, huku wapinzani wakigawana asilimia 8.28 zilizobaki.
Licha ya uchaguzi huo wa juzi kugubikwa na kasoro nyingi, upinzani umeonekana kuchomoza huku katika baadhi ya mikoa ukipata ushindi maradufu hasa katika maeneo ambayo una nguvu kubwa wakati katika maeneo ambayo ulikuwa na viti vichache au kutokuwa navyo kabisa, umeibuka na kuipokonya CCM baadhi ya mitaa na vijiji.
Vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) yaani Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi vimejizolea viti vingi tofauti na awali, huku chama kipya cha ACT kikichomoza na kupata ushindi katika maeneo kadhaa ya mikoa ya Kigoma na Katavi.
Mikoa ambayo upinzani umeonekana kuzoa viti vingi ni Arusha, Kilimanjaro, Mbeya, Iringa, Kigoma, Mara, Kagera na Dar es Salaam, hali ambayo wachunguzi wa mambo wameielezea kuwa siyo dalili njema kwa CCM.

Kikwete atakiwa kuwachukulia hatua wahusika Escrow

Mashirika ya kigeni pamoja na nchi wafadhili wa Tanzania zimemtaka Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa nchi hiyo kuwachukulia hatua maafisa waandamizi wa serikali waliotajwa kuhusika na kashfa ya wizi ya Escrow.
Baadhi ya nchi zimetishia kusitisha misaada yao kwa Tanzania hadi pale kadhia hiyo itakapotatuliwa na wahusika kuwajibishwa. Marekani ambayo ni moja ya nchi wafadhili imetahadharisha kuwa itazuia msaada wa dola milioni 700 ambazo ni sawa na shilingi trilioni 1.1 za Tanzania kutokana na kashfa ya Tegeta Escrow.
Marekani imesema, mkataba wa pili wa miradi inayofadhiliwa na shirika la nchi hiyo la Changamoto za Milenia (MCC) utategemea hatua zitakazochukuliwa na serikali ya Tanzania dhidi ya wahusika wa kashfa hiyo.
Hayo yanajiri wakati Rais Jakaya Kikwete akisubiriwa kutoa maamuzi ya mapendekezo yaliyofikiwa na Bunge kuhusiana na sakata la wizi wa fedha zaidi ya Sh. bilioni 300 kutoka akaunti ya Tegeta Escrow wiki ijayo.
Baadhi ya nchi za Ulaya pia zimemtaka Rais Kikwete kuchukua hatua za haraka dhidi ya wahusika wa kashfa hiyo ya ufisadi la sivyo misaada kwa Tanzania itasimamishwa.

Muswada wa sheria ya usalama wapitishwa Kenya

Muswada wenye utata wa marekebisho ya sheria ya usalama umepitishwa bungeni nchini Kenya baada ya mijadala na malumbano ya mchana kutwa kati ya wabunge wa serikali na wale wa upinzani. Kikao maalumu cha bunge cha kujadili marekebisho ya sheria ya usalama kilivurugika mara kadhaa leo Alhamisi baada ya wabunge wa upinzani kuzusha rabsha ndani ya bunge na kutatiza kabisa shughuli za taasisi hiyo. Spika wa bunge la Kenya, Justin Muturi, alifanya juhudi kubwa za kuwatuliza wapinzani na hata kuahirisha kwa muda kikao hicho lakini kila wakati wabunge waliporudi ukumbini, fujo zilianza tena. Upinzani umelalamikia kupitishwa muswada huo ingawa kumekuweko na marekabisho kadhaa kwenye vipengee vilivyokuwa na utata.
Muungano wa upinzani wa CORD unapinga marekebisho ya sheria mpya ya usalama kwa madai kwamba mabadiliko hayo yatairudisha Kenya katika enzi za udikteta na utawala wa kipolisi. Mabadiliko hayo pia yamepingwa na makundi ya kiraia na yale ya kutetea haki za binadamu kwa madai kuwa yatatoa mwanya kwa vyombo vya usalama kukiuka haki za binadamu. Serikali imesema sheria hiyo ndiyo wenzo pekee unaweza kuisaidia kukabiliana na hali ya ukosefu wa usalama katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Katika hatua nyingine, bunge la Kenya limemuidhinisha Waziri mpya wa Mambo ya Ndani, Joseph Nkaissery, ambaye aliteuliwa na Rais Uhuru Kenyatta juma lililopita. Wabunge wa serikali na wale wa upinzani wamemuidhinisha Nkaissery ambaye sasa ataidhinishwa rasmi na Rais kabla ya kuapishwa. Nkaissery anachukua nafasi ya mtangulizi wake aliyefutwa kazi, Joseph Ole Lenku

JK atunukiwa PHD katika mahafali ya pili ya Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela jijini Arusha leo


  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambae pia ni Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akimtunuku shahada ya heshima ya Uzamivu PhD Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Profesa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kutambua mchango wake katika Jamii, kitaifa na kimataifa pamoja na kufanikisha kuanzishwa kwa Taasisi hiyo kwenye Mahafali ya pili  iliyofanyika leo  jijini Arusha. Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambae pia ni Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akimtunuku shahada ya PhD ya Sayansi Uhandisi na Hesabu Bw. James Philip kwenye Mahafali ya pili ya Taasisi hiyo iliyofanyika leo jijini Arusha.
 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambae pia ni Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akihutubia kwenye Mahafali ya 2 ya Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela iliyofanyika leo jijini Arusha. Sehemu ya wahitimu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela  Wahadhiri katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanmzania ambae pia ni Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akiwa katika maandamano na viongozi wa Taasisi hiyo pamoja na wahitimu, wakati wa Mahafali ya 2 ya Taasisi hiyo yaliyofanyika leo  jijini Arusha. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambae pia ni Mkuu wa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal na wakiwa katika picha ya pamoja na wahitimu wa Shahada ya Uzamili na Uzamifu kwenye Mahafali ya 2 ya Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela iliyofanyika leo jijini Arusha

Friday, 12 December 2014

Marekani yacharuka escrow;Tanzania yakosa mabilioni ya MCC, ni Dola 450 milioni


 
Dar es Salaam. Wakati Serikali ya Marekani ikisema haitatoa fedha za Changamoto za Milenia (MCC) hadi utekelezaji wa maazimio ya Bunge kuhusu ufisadi katika akaunti ya Tegeta Escrow wa Sh306 bilioni utakapofanyiwa kazi, Ikulu imesema, Rais Jakaya Kikwete hatatekeleza agizo hilo kwa shinikizo la msaada huo.
MCC ni taasisi ya Serikali ya Marekani inayotoa misaada kwa nchi zinazoendelea. Shughuli za MCC zinajengwa katika msingi kwamba msaada utaleta ufanisi na matokeo makubwa zaidi pale tu unapoimarisha utawala bora, uhuru wa kiuchumi na uwekezaji katika watu ambao unakuza uchumi na kuondoa umaskini.
Taarifa hiyo ilisema Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la MCC kupitia taarifa yake kwa umma iliyotolewa jana na Ubalozi wa Marekani nchini ilisema, katika mkutano wa bodi hiyo uliokutana Desemba 10 mwaka huu nchini Marekani, ulielezea hofu na masikitiko kuhusu hali ya rushwa inavyoendelea Tanzania.
Fedha ambazo Tanzania ilipaswa kupata kupitia mradi huo wa MCC awamu ya pili ni Dola 450 milioni ambazo ni sawa na Sh765 bilioni.
“Japokuwa bodi ilipiga kura ya kuiruhusu Tanzania iendelee na maandalizi kwa ajili ya mkataba wa pili kwa dhati kabisa, inaihimiza serikali ya Tanzania kuchukua hatua thabiti na mahsusi za kukabiliana na rushwa kama sharti la msingi kwa bodi hiyo kufanya uamuzi wa mwisho wa kuidhinisha mkataba huo.
“Bodi ilieleza kutambua umuhimu wa kusubiri na kuona utekelezaji kamilifu wa tamko lililotolewa na Ikulu ya Tanzania hapo Desemba 9 mwaka huu kwamba itachukua hatua za haraka na kutoa uamuzi dhahiri na thabiti kuhusu maazimio ya Bunge juu la suala la IPTL,” ilieleza taarifa hiyo.
Katika tamko hilo kwa umma, Balozi wa Marekani nchini, Mark Childress alisema “Kupigwa hatua katika mapambano dhidi ya rushwa ni muhimu sana kwa mkataba mpya kati ya MCC na Tanzania na katika kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara Tanzania.”
Aliongeza: “Tunatoa wito kwa serikali kuchukua hatua za haraka kuhusu suala hili hasa kutokana na uzito wake katika masuala muhimu kadhaa ya maendeleo,” ilisema taarifa hiyo.
Hali kadhalika, Bodi iligusia makubaliano kadhaa yaliyofanyika na Tanzania iliahidi kufanya mageuzi ya kisera, kimuundo na kitaasisi ili kuongeza ufanisi na uwazi katika taasisi zake na katika sekta ya nishati.
Balozi Childress aliendelea kusema, “Tunafurahi kwamba mchakato wa majadiliano ya maandalizi ya mkataba wa pili utaendelea kwa miezi kadhaa ijayo. Tunapenda kusisitiza kuwa ni lazima ahadi hizi zitekelezwe kabla Marekani haijafanya uamuzi wa mwisho kuhusu mkataba wowote mpya na Tanzania.”
Katika mkutano huo, Tanzania ilikuwa miongoni mwa nchi 10 zilizojadiliwa na Bodi ya MCC iliyokutana kuangalia kama nchi hizi zimekidhi vigezo vya kuendelea na mchakato wa kuandaa mikataba mipya.
Iwapo mkataba huo utapitishwa, utakuwa wa pili wa MCC kwa Tanzania kati ya mwaka 2008 na 2013 ambao ulitekeleza mkataba wa uwekezaji wenye thamani ya Dola za milioni 698 sawa na Sh1.18 trilioni ambao uliowezesha utekelezaji wa miradi ya maji, barabara na nishati ya umeme nchini kote Tanzania
Chini ya mkataba huo, mtandao wa nyaya za umeme wenye zaidi ya kilomita 3,000 ulijengwa, jumla ya kilomita 450 za barabara pia zilijengwa, kadhalika mitambo mikubwa miwili ya usafishaji maji na njia ya kurukia ndege katika kiwanja kimoja cha ndege ilijengwa.
Kauli ya Ikulu
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alisema hilo ni jambo la kawaida kwani ili uweze kupata msaada huo ni lazima uwe umetimiza masharti na vigezo ambavyo miongoni ni masuala ya utawala bora na rushwa.
“Kabla ya kutia saini wanaangalia masuala ya utawala bora na rushwa na kama walivyosema wanasubiri kuona utekelezaji wake ni jambo la kawaida duniani kutokea.”
Kuhusu Rais Jakaya Kikwete kuchukua hatua za haraka dhidi ya waliohusika na sakata hilo, Balozi Sefue alisema, “MCC ipo au haipo Rais (Kikwete) anachukulia suala hili kwa umakini na atachukua uamuzi kwa misingi ya ushahidi uliotolewa.”
EIL yakazia
Wakala wa Uchunguzi wa Mazingira (EIA) wameitaka MCC kutokubali kuidhinisha mkabata huo na Tanzania wa dola 450 milioni hadi Rais Kikwete atakapochukua hatua stahiki dhidi ya vitendo vya rushwa viliyotawala kwenye sakata la ujangili na usafirishwaji wa pembe za ndovu kwenda nje ya nchi hususani China.
Taasisi hiyo inayojihusisha na masuala ya mazingira ilitoa wito huo jana kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry na Mwenyekiti ambaye pia ni Mkurugenzi wa MCC, Diana Hyde kwamba wasitishe hatua hiyo kwa Tanzania.
Kutokana na hilo, EIA imeomba MCC ambayo imekuwa ikifadhili miradi ya maendeleo nchini kusitisha hatua hiyo kwanza hadi Rais Kikwete atakapolivalia njuga suala hilo.
Novemba mwaka huu, EIA ilitoa ripoti ya utafiti wa ujangili uliyoanika madudu dhidi ya mauaji ya tembo na namna meno yanavyotoroshwa nchini.
Mvutano bungeni
Katiba Bunge la 16/17 lililomalizika mjini Dodoma mwishoni mwa mwezi uliopita, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya walivutana kuhusu ufadhili huo wa MCC uliokwama kutokana na ufisadi wa akaunti ya Tegeta Escrow.
Wakati wabunge wakiomba kiti cha Spika kiruhusu kujadiliwa bungeni kwa ripoti ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu ufisadi wa akaunti ya Tegeta Escrow, Mnyika alisimama na kusema, “kama ripoti hii haitajadiliwa basi fedha zinazotolewa na MCC tutazikosa.”
Baada ya kauli hiyo, Mkuya alisimama na kusema, “Si kweli kwamba tutazikosa fedha hizo kwani taratibu zinaendelea vizuri na mkataba utasainiwa Desemba mwaka huu na fedha hizo zitatoka Desemba.”
Kafulila
Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila akizungumzia uamuzi huo wa bodi ya MCC alisema, “taarifa hiyo imekuja wakati mwafaka...imenivisha nguo baada ya kuwa nimevuliwa bungeni na kuitwa mimi mwongo.”
Alisema, “Nilisema bungeni kwamba hasara tunayoipata kutokana na ufisadi huo wa Escrow ni zaidi kwani misaada tuliyokuwa tunaisubiri ya Sh900 bilioni kutoka Ulaya, Marekani Dola milioni 700 na ukijumuisha Sh306 bilioni ni zaidi ya Sh2 trilioni.”
Kafulila alisema fedha hizo zilikuwa zitoke tangu Septemba mwaka huu kama ambavyo Ghana imezipata lakini kutokana na uzembe wa Serikali ya Tanzania, imepoteza kiasi hicho cha fedha.
“Waziri wa fedha (Saada Mkuya) na Profesa Muhongo (Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo) walikana bungeni kwamba ninasema uwongo sasa ukweli umejulikana nani ni mkweli na nani ni mwongo,” alisema Kafulila jana

Watu milioni 20 kushiriki Arubaini ya Imam Hussein (as)

Maafisa wa serikali ya Iraq wamesema kuwa inakadiriwa watu milioni 20 watashiriki katika maombolezo ya siku ya Arubaini ya mjukuu wa Mtume Muhammad (saw) Imam Hussein (as) katika mji mtakatifu wa Karbala Jumamosi ya kesho.
Waislamu wa madehebu ya Shia kutoka nchi mbalimbali dunia wanaendelea kuwasili katika mji huo mtakatifu kwa njia mbalimbali za usafiri wa anga na nchi kavu kukumbuka siku ya Arubaini na tukio chungu la kuuawa shahidi mjukuu wa Mtume Muhammad (saw) akigapania dini ya Mwenyezi Mungu na matukufu ya kibinadamu hapo mwaka 61 Hijria. Serikali ya Iraq imetangaza kuwa hadi sasa Waislamu milioni 17 wamewasili mjini karbala na kwamba inatarajiwa kuwa idadi ya watu wanaokwenda kuzuru kaburi la Imam Hussein itafikia milioni 20 hadi Jumamosi ya kesho.
Jeshi la Iraq limeimarisha usalama katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo hususan mjini Karbala kwa kuhofia mashambulizi ya kundi la kigaidi na kiwahabi la Daesh.
Maombolezo ya siku ya Arubaini hufanyika kila mwaka baada ya kupita siku Arubaini tangu tarehe 10 mwezi wa Muharram kwa ajili ya kukumbuka mauaji ya Imam Hussein AS na masahaba zake 72 ambao walijitolea roho zao kwa ajili ya kuhuisha dini ya Mwenyezi Mungu katika jangwa la Karbala mnamo mwaka 61 Hijria

Rais wa Kenya atoa onyo kwa waungaji mkono wa ugaidi

Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya leo Ijumaa ameliongoza taifa kuadhimisha miaka 51 ya uhuru wa nchi yake.
Sherehe hizo zilizojaa mbwembwe zilifanyika katika uwanja wa Nyayo jijini Nairobi na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali wakiwemo Marais Yoweri Museveni wa Uganda, John Dramani Mahama wa Ghana na Paul Kagame wa Rwanda. Viongozi wa muungano mkuu wa upinzani wa CORD nchini Kenya pia walihudhuria sherehe hizo.
Akizungumza kwenye hotuba yake, Rais Kenyatta amesema ugaidi ni tatizo la kimataifa na kusisitiza kuwa, vita dhidi ya ugaidi vinapaswa kuendeshwa kwa ushirikiano wa kila nchi duniani. Rais wa Kenya amewataka Wakenya kuisaidia serikali kukabiliana na changamoto za kiusalama hususan ugaidi wa kundi la al-Shabab la Somalia. Kiongozi huyo amewaonya wale wanaoshirikiana na magaidi akisema chuma chao ki motoni. Amekanusha madai kwamba vita dhidi ya Ugaidi vinawalenga Waislamu na kusisitiza kuwa Waislamu ni wapenda amani na wanafaa wawakatae wanaojaribu kutumia dini yao kutenda vitendo vya kinyama dhidi ya Wakenya. Kundi la al-Shabab limekuwa likifanya mauaji ya kinyama dhidi ya raia wasio na hatia nchini Kenya kama njia ya kuishinikiza serikali ya Nairobi iondoe jeshi lake nchini Somalia.

Ayatullah Khatami: Mateso ya CIA ni unyama mkubwa

Khatibu wa muda wa Sala ya Ijumaa hapa mjini Tehran amesema leo kuwa, ripoti iliyotolewa wiki hii na Baraza la Seneti nchini Marekani ni ya kushtua. Ripoti hiyo imefichua jinsi Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) lilivyowatesa kinyama washukiwa wa ugaidi katika jela la Guantanamo miaka kadhaa iliyopita. Ayatullah Ahmad Khatami amesema mateso hayo ya CIA dhidi ya washukiwa wa ugaidi ni unyama na ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu. Ayatullah Khatami amesema inasikitisha kuona Marekani ikijigamba kuwa inatetea haki za binadamu duniani ilihali nchi hiyo ndiyo mkiukaji nambari moja wa haki hizo. Khatibu wa Sala ya Ijumaa hapa Tehran pia amelaani mauaji ya Waziri wa Palestina, Ziad Abu Ein aliyeuawa shahidi siku ya Jumatano na jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel. Ayatullah Ahmad Khatami amesema serikali ya Umoja wa Kitaifa ya Palestina inapaswa kuchukua hatua kali dhidi ya Israel kufuatia jinai hiyo. Amesema kwa mara nyingine tena Wazayuni wameonyesha udhalimu na unyama wao hadharani na kusisitiza kuwa muqawama na mapambano ya Wapalestina ndiyo njia pekee ya kumshinda adui mzayuni.

Rais Mugabe awateua mawaziri 8 wapya

Siku chache baada ya Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe kumfuta kazi makamu wake Joyce Mujuru na mawaziri wanane, kiongozi huyo amewateua na kuwaapisha shaksia wengine kujaza nafasi hizo za uwaziri baada ya kufanya mabadiliko machache kwenye baraza la Mawaziri.
Emmerson Mnangagwa ambaye siku chache zilizopita aliteuliwa kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais ataendelea pia kushikilia wadhifa wake wa Waziri wa Sheria. Baadhi ya mawaziri waliobadilishwa ni pamoja na Oppah Muchinguri ambaye ametolewa kwenye Wizara ya Wanawake na Maendeleo ya Jamii na kupelekwa Wizara ya Elimu ya Juu.
Rais Mugabe alimfuta kazi makamu wake Joyce Mujuru na mawaziri 8 siku ya Jumanne iliyopita baada ya kuwatuhumu kuwa walikuwa wakipanga njama ya kumuua. Hatima ya Mujuru na wenzake waliotimuliwa bado haijabainika.

Ripoti: Magaidi wa Syria wameua zaidi ya raia 300 Aleppo

Shirika la kutetea haki za binadamu la Syrian Observatory for Human Rights limesema kuwa magaidi wa Syria wamewaua raia wasiopungua 311 kati ya mwezi Julai na Disemba mwaka huu katika mkoa wa Aleppo ulioko kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
Shirika hilo limesema kwenye ripoti yake mpya kuwa, wanawake 25 na watoto 42 ni miongoni mwa raia wasio na hatia waliouawa na magaidi hao. Ripoti hiyo inasema magaidi wamekuwa wakitumia silaha zilizopigwa marufuku kwenye vita vya Syria. Taarifa ya shirika hilo lenye makao yake mjini London, Uingereza, imelaani mauaji ya raia na kuvitaka vyombo vya kimataifa kuchunguza kadhia hiyo na kuwachukulia hatua wahusika.
Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonyesha kuwa, takriban watu laki mbili wameuawa na mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi kutokana na vita nchini Syria. Mgogoro wa Syria umeshindwa kutatuliwa kwa njia za kidiplomasia kutokana na uungaji mkono mkubwa wa Wamagharibi na Wazayuni kwa makundi ya kigaidi yanayopigana na serikali ya Rais Bashar Asad wa nchi hiyo.

Rais wa Afghanistan awaarifisha mawaziri 4 muhimu

Serikali mpya ya Afghanistan imeanza kupata sura baada ya Rais Ashraf Ghani kuwaarifisha mawaziri wanne muhimu.
Rais Ghani leo Ijumaa amewaarifisha Muhammad Mastur (Fedha), Mujghan Mustafawi (Masuala ya Wanawake), Muzamil Shinawari (Biashara) na Atikullah Atif Mal kama Waziri wa Mambo ya Nje. Hatua hiyo ya Rais mpya wa Afghanistan imechukuliwa baada ya kupita zaidi ya mwezi mmoja tangu kiongozi huyo akubali kugawana madaraka na mpinzani wake Abdullah Abdullah baada ya wawili hao kupinga matokeo ya duru ya pili ya uchaguzi wa rais nchini humo.
Duru zinaeleza kuwa, Serikali mpya ya Afghanistan itakuwa na jumla ya mawaziri 25 ambapo Rais Ashraf Ghani atateua 13 kati yao huku 12 wakiteuliwa na Abdullah Abdullah ambaye kwa sasa ndiye Afisa Mkuu Mtendaji wa Serikali (CEO). Mawaziri walioteuliwa watatakiwa kuidhinishwa na Bunge kabla ya kuanza rasmi kazi zao

Kuanza kesi ya Simone Gbagbo, mke wa rais wa zamani wa Ivory Coast

Simone Gbagbo Simone Gbagbo
Kesi inayomkabili Simone Gbagbo mke wa rais wa zamani wa Ivory Coast anayetuhumiwa kuvuruga usalama nchini humo, ilianza jana Jumanne katika mji mkuu wa kiuchumi wa nchi hiyo, Abidjan. Wakili wa Simone Gbagbo amesema ana matumaini kesi hiyo itafanyika kwa uadilifu. Inasemekana kuwa, mke huyo wa raia wa zamani wa Ivory Coast amehamishwa kutoka kaskazini hadi kusini mwa mji huo kwa ajili ya kesi hiyo. Bi. Simone Gbagbo anatuhumiwa pia na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) kutenda jinai dhidi ya binadamu, na mahakama hiyo imetaka ikabidhiwe mtuhumiwa huyo. Hata hivyo serikali ya Ivory Coast sambamba na kusisitiza kuwa mahakama za nchi hiyo zina uwezo wa kuhukumu kiadilifu, imejiepusha kumkabidhi mwanamama huyo.
Wapinzani wa serikali ya Ivory Coast wanasisitiza kuwa Laurent Gbagbo hana hatia na wanataka arejeshwe nchini humo. Tangu Novemba 31 mwaka 2011 kiongozi huyo wa zamani anashikiliwa na mahakama ya The Hague kwa tuhuma za kutenda jinai dhidi ya binadamu. Inaonekana kuwa, viongozi wa Ivory Coast wanalipa kipaumbele suala la kuimarisha amani na utulivu nchini na wanafanya jitihada za kuwavutia wapinzani hasa katika kipindi hiki cha kukaribia uchaguzi uliopangwa kufanyika mwakani.
Weledi wa mambo wanaamini kuwa, kutokana na hali tata ya sasa, itakuwa vigumu kwa rais wa sasa wa nchi hiyo Alassane Ouattara kushinda katika uchaguzi ujao wa mwaka 2015. Nchi ya Ivory Coast imekuwa ikisumbuliwa na mapigano ya hapa na pale ya kikabili baada ya Ouattara kuchukua hatamu za uongozi. Wachambuzi wa masuala wa kisiasa wanasema kuwa, mwenendo huo unaweza kuitumbukiza tena Ivory Coast katika machafuko ya ndani.
Kwa upande mwingine kushtadi malalamiko ya jumuiya za wafanyakazi ya kupinga umasikini katika jamii, ni kadhia nyingine iliyopunguza umaarufu wa Alassane Ouattara. Inasemekena kuwa, kukithiri umasikini kumeathiri nyanja zote za kimaisha ikiwemo sekta ya afya, lishe, elimu na makazi ya wananchi wa Ivory Coast.
Tatizo jingine linalozididisha hali ya ukosefu wa usalama nchini humo ni kuwepo idadi kubwa ya silaha mikononi mwa raia. Tangu wakati wa uasi wa mwaka 2002 na vita vya ndani vya mwaka 2010 hadi 2011, takriban silaha nyepesi laki moja zimebakia mikononi mwa raia. Baadhi wanasema kuwa, silaha hizo ndizo zinazosababisha machafuko na mauaji nchini Ivory Coast. Hivi karibuni taasisi moja ya Afrika iliitaka serikali ya Abidjan ifanye jitihada zaidi kwa ajili ya kuharakisha mwenendo wa kukusanya silaha nyepesi miongoni mwa raia.
Weledi wa mambo wanasema kwamba, viongozi wa nchi hiyo, wanajitahidi kulegeza misimamo na kutochukua hatua kali dhidi yawapinzani kwa kuzingatia hali ya mambo inayotawala nchini humo. Hasa kwa kuwa, chama cha upinzani cha Ivorian Popular Front (IPF) ambacho kinaendelea kumuunga mkono Gbagbo huenda kikawa na taathira katika matokeo ya uchaguzi ujao. Kwa kuzingatia hayo yote, baadhi wanaamini kuwa, ni jambo lililo mbali kuwa Simone Gbagbo atapewa adhabu kali kupitia kesi hiyo inayomkabili

Msimamo wa Iran kuhusu silaha za mauaji ya umati katika mkutano wa Vienna

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ikiwa miongoni mwa wahanga wa silaha za mauaji ya umati, inaamini kuwa kumiliki silaha hizo hakudhamini usalama wa nchi yoyote ile. Hayo yameelezwa na Reza Najafi, mwakilishi wa Iran katika Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA), kwenye mkutano wa kimataifa wa Vienna uliojadili taathira za kutumiwa silaha za nyuklia kwa binadamu. Amesisitiza kuwa, dhamana pekee ya kukabiliana na vitisho vya silaha hizo ni kutokomezwa kikamilifu chini ya udhibiti mkali wa kimataifa. Najafi ameongeza kuwa, tangu yalipojiri mashambulio ya Marekani dhidi ya watu wa Hiroshima na Nagasaki huko Japan, mwanadamu amekuwa akiishi kwa hofu na woga wa silaha za nyuklia. Amesema, suala la baadhi ya nchi kumiliki silaha hizo halikubaliki na kwamba linapaswa kulaaniwa, kwani ni kinyume na Mkataba wa Kuzuia Uzalishaji na Usambazaji wa silaha za Nyuklia (NPT).
Kuwepo maelfu ya vichwa vya mabomu ya nyuklia na kuzalisha silaha za kisasa za aina hiyo kunahesabiwa kuwa tishio kwa mwanadamu. Katika eneo la Mashariki ya Kati pia Israel ambayo ni utawala pekee kwenye eneo hilo unaomiliki silaha za nyuklia, inahatarisha amani ya eneo hilo kwa kuwa na mabomu kati ya 200 hadi 400 ya nyuklia.
Kwa kuzingatia wasiwasi huo, nchi nyingi zikiwemo zile za Jumuiya ya Nchi Zisiyofungamana na Siasa za Upande Wowote (NAM) zinasisitiza kutekelezwa kikamilifu na bila ubaguzi mkataba wa NPT.
 Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia sambamba na kukaribisha jitihada za pande zote za kutokomezwa silaha za atomiki duniani kote tangu huko nyuma ilipendekeza kutokomeza silaha hizo katika Mashariki ya Kati, na kuunga mkono suala hilo. Vilevile Iran imetoa pendekezo la kufanyika kongamano la kuangamizwa silaha za nyuklia Mashariki ya Kati lakini Marekani imezuia kufanyika kongamano hilo.
Katika hotuba yake kwenye mkutano wa Vienna, mwakilishi wa kudumu wa Iran katika wakala wa IAEA ameashiria matamshi ya Kiongozi Muadhamu katika ufunguzi wa mkutano wa 16 wa viongozi wa NAM mjini Tehran Oktoba 30 mwaka 2012, ambapo alisema kuwa Jamhuri ya Kiislamu inaamini kwamba matumizi ya silaha za nyuklia, kemikali na nyinginezo kama hizo ni dhambi kubwa isiyosameheka.
 Ripoti zilizotolewa zinasema, inakadiriwa kuwa katika muongo ujao, gharama za kuzalisha silaha zaidi za nyuklia na mitambo inayohusiana na silaha hizo itafikia dola trilioni moja. Mkutano wa kimataifa wa Vienna  uliojadili taathira za silaha za nyuklia kwa binadamu pengine ni fursa nzuri ya kukumbusha kwa mara nyingine wasiwasi wa walimwengu kuhusu silaha hizo, lakini hatupaswi kusahau kuwa, kufanikishwa dhana ya kuwa na dunia isiyo na silaha za nyuklia kunapaswa kuanzia katika nchi ambazo zinaamini kwamba kuwa na silaha hizo kunazisaidia kiusalama.
Kwa msingi huo nchi zinazomiliki silaha hizo zinapaswa kuchukua hatua za mwanzo kuhusu suala hilo, la sivyo jitihada au mikataba na makubaliano yanayofanyika kuhusu suala hilo hayatakuwa na natija yeyote. Kama sera za kijeshi na kiusalama za nchi zinazomiliki silaha za atomiki zitaendelea kutegemea mlingano wa nguvu wa silaha za nyuklia, itakuwa vigumu kuchukuliwa hatua za maana katika uwanja huo.
Ni kwa msingi huo ndiyo maana mwakilishi wa Iran katika wakala wa IAEA amezitaka nchi zinazomiliki silaha za nyuklia kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa mkataba wa N.P.T na kuacha kuzidisha silaha hizo, kuzalisha vizazi vipya au kupeleka silaha hizo katika nchi nyingine.

Umoja wa Mataifa: Mapambano dhidi ya waasi yatachukua muda mrefu mashariki mwa DRC

Umoja wa Mataifa ulitangaza jana kuwa, mapambano dhidi ya makundi ya wanamgambo waasi na yale yanayosababisha ghasia na machafuko yatachukua muda mrefu huko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Hivi sasa, viongozi wa serikali ya Kongo pamoja na wale wa Umoja wa Mataifa wanalinyooshea  kidole cha lawama kundi la waasi wa ADF NALU wa nchini Uganda kwa kusababisha ukosefu wa amani na utulivu nchini Kongo. Hayo yanajiri katika hali ambayo, Martin Kobler, Mkuu wa Operesheni za kikosi cha Umoja wa Mataifa nchini Kongo MONUSCO hajatangaza kinagaubaga kama kundi la ADF NALU limehusika na machafuko yanayoendelea mashariki mwa nchi hiyo. Imeelezwa kuwa, waathiriwa wa mashambulio ya waasi yaliyoanza mwezi Oktoba hadi sasa katika mji wa Beni ulioko katika jimbo la Kivu Kaskazini, mashariki mwa Kongo imefikia watu 250. Waasi wa ADF wamejikita mashariki mwa Kongo tokea mwaka 1995. Baadhi ya ripoti zinaeleza kuwa kundi hilo la waasi wa Uganda lilihusika na mauaji ya watu wasiopungua 13 yaliyofanywa siku za Jumamosi na Jumapili iliyopita huko mashariki mwa Kongo. Kabla ya hapo, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio lililopendekezwa na Ufaransa na Uingereza la kuitaka serikali ya Kongo iwatimue waasi walioko mashariki mwa nchi hiyo. Kuhusiana na kadhia hiyo, wanachama wa kudumu na wasio wa kudumu wa baraza hilo walitoa taarifa ya kuunga mkono kuwepo hali ya utulivu na amani nchini humo, na kusisitiza suala la  kupokonywa silaha waasi hao. Hata hivyo, ADF NALU sio kundi pekee la waasi linalosababisha ukosefu wa amani na utulivu katika eneo la mashariki mwa Kongo, kwani licha ya waasi hao wa Uganda, kundi jingine la waasi wa Kihutu la Democratic Forces for the Liberation of Rwanda 'FDLR' la nchini Rwanda linalovuruga amani na utulivu nchini Kongo. Makundi hayo yamekuwa yakiwatumia watoto kwenye medani za vita na hata kuwadhalilisha kijinsia watoto na wanawake katika nchi hiyo.  Wahutu wa Rwanda walikimbilia  nchini Kongo  kwenye muongo wa 1990  na kuunda kundi la waasi, na imeelezwa kuwa, idadi kubwa ya wanamgambo wa kundi hilo ni watu waliohusika na mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 nchini Rwanda. Hii ni katika hali ambayo, wataalamu wengi wanaamini kwamba, propaganda kubwa zinazofanywa na madola ya Magharibi kuwa zinashirikiana na Kongo kwa lengo la kurejesha amani na utulivu nchini humo,  ni mchezo wa kisiasa tu na wala nchi hizo hazina azma  thabiti ya kurejesha amani katika eneo la mashariki mwa Kongo. Kwa hakika viongozi wa Magharibi, wao wenyewe ndiyo wasababishaji wakuu wa  machafuko na mapigano barani Afrika na hasa nchini Kongo ili waweze kuendelea kubaki kijeshi kwenye maeneo mbalimbali na kupora maliasili na utajiri wa nchi hizo. Wadadisi wa mambo wanaeleza kuwa, mashirika ya kigeni yakiwa na lengo la kupora maliasili na utajiri wa Kongo, yanataka machafuko na mapigano yaendelee nchini humo. Nazo nchi za eneo la Maziwa Makuu ya Afrika zinajaribu kulinda maslahi yao kwa kuendelea machafuko mashariki mwa Kongo. Kabla ya hapo, Umoja wa Mataifa uliunda jopo la wataalamu la kuchunguza mgogoro wa Kongo, na kutoa ripoti iliyokuwa ikizituhumu nchi za Rwanda na Uganda kuwa zinawapatia silaha waasi, kuwachochea wanajeshi wa serikali ya Kinshasa watoroke jeshini pamoja na kuwapatia waasi hao msaada wa kiintelijinsia. Katika hali kama hiyo, hatua ya Umoja wa Mataifa ya kutangaza kuendelea mapigano na mapambano dhidi ya makundi ya waasi mashariki mwa Kongo, inaweza kuwa ni tahadhari na indhari ya kukaririwa majanga ya kibinadamu  katika eneo hilo.

Ansarullah ya Yemen yapinga mpango wa Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi

Nchi wanachama wa Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi (PGCC) ambazo mwaka 2011 ziliingilia kati mgogoro wa Yemen na kuzuia mapinduzi ya wananchi wa nchi hiyo kupata ushindi, kwa mara nyengine tena, hivi sasa zinafanya kila njia ili kuzima tena wimbi la mabadiliko ya kisiasa lililoanza nchini humo tangu mwezi Julai mwaka huu. Katika taarifa iliyotolewa mwishoni mwa kikao cha 35 cha Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi kilichofanyika siku ya Jumanne katika mji mkuu wa Qatar, Doha nchi wanachama wa PGCC zimetaka wapiganaji wa Kihouthi wa Kamati za Wananchi waondoke katika mji mkuu wa Yemen, Sana’a na katika maeneo mengine yanayodhibitiwa na wapiganaji hao.
Ali Abdullah Saleh, ambaye kuanzia mwaka 1978 hadi 1990 alikuwa Rais wa Yemen ya Kaskazini, na kuanzia mwaka 1990 hadi mwaka 2011 alikuwa Rais pia wa Yemen iliyoungana, kama ilivyokuwa kwa watawala wa aghalabu ya nchi za Kiarabu za Mashariki ya Kati na za kaskazini mwa Afrika, mwaka 2011 naye pia alikabiliwa na wimbi kubwa la upinzani wa wananchi. Japokuwa Saleh alijaribu kuzima wimbi hilo la upinzani ili aweze kuendelea kubakia madarakani, lakini wananchi wa Yemen walishikilia msimamo wao kuhakikisha dikteta huyo anang’atuka madarakani. Licha ya hatua alizochukua Ali Abdullah Saleh mwenyewe, baadhi ya watawala wa nchi za Kiarabu za eneo, nao pia walijaribu kufanya juu chini ili kumwokoa dikteta huyo na gharika ya mapinduzi ya wananchi wa Yemen. Baadhi ya nchi wanachama wa PGCC na hasa Saudi Arabia ilikuwa moja ya viranja wakuu wa kumlinda Saleh na kuhakikisha anaendelea kushika hatamu za utawala, lakini nguvu na ukubwa wa wimbi la upinzani wa wananchi dhidi ya dikteta huyo, ziliulazimisha utawala wa kifalme wa Aal Saud ufikirie mbinu na hila nyengine kupitia PGCC ili kupotosha mkondo wa mapinduzi ya wananchi wa Yemen. Kulingana na mpango huo Ali Abdullah Saleh aling’atuka madarakani kwa sharti la kutoshtakiwa na kufatiliwa kisheria kwa jinai alizotenda, na akakabidhi madaraka kwa makamu wake Abd Rabbuh Mansur Hadi, kupitia uchaguzi wa kimaonyesho uliofanyika nchini humo. Mbinu na hila ya mpango wa Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi ulipotosha mkondo wa mapinduzi ya wananchi wa Yemen na kuwatumbukiza wananchi hao kwenye lindi la hali ya mchafukoge wa kisiasa iliyoendelea kwa muda wa miaka mitatu. Kushadidi hali hiyo na udhaifu mkubwa wa kiutendaji ulioonyeshwa na serikali ya mpito ya Abd Rabbuh Mansur Hadi, viliwafanya wananchi, wakiongozwa na harakati ya Mahouthi ya Ansarullah waanzishe wimbi jipya la maandamano dhidi ya serikali hiyo. Kushadidi na kuendelea wimbi hilo la maandamano ya upinzani lililoanza mwezi Julai mwaka huu hatimaye kuliipigisha magoti serikali ya Mansur Hadi, ambapo mnamo mwezi Septemba ilikubaliana na matakwa ya wananchi likiwemo la kujiuzulu serikali na kuundwa serikali mpya kwa maafikiano na harakati ya Ansarullah. Hata hivyo maafikiano hayo hayakukubaliwa na baadhi ya nchi wanachama wa PGCC hususan Saudi Arabia na Imarati. Kwa mtazamo wa Saudia, kuundwa serikali itakayotoa nafasi kuu kwa Ansarullah na kuifanya harakati hiyo iwe na sauti kubwa katika matukio ya Yemen ni tishio dhidi ya mipaka yake na pia kunaitia hofu na wasiwasi Riyadh juu ya kujitokeza mlingano mpya wa nguvu katika eneo. Wapinzani wa Ansarullah katika eneo wanaitakidi kuwa kupata nguvu harakati hiyo ambayo waungaji mkono wake waliowengi ni Mashia wa Zaidiyyah kutazipa nguvu zaidi harakati nyengine za kupinga tawala za kifalme katika nchi nyengine za Kiarabu na kuongezeka satua na ushawishi wa Iran nchini Yemen. Kwa sababu hiyo nchi wanachama wa PGCC zimetoa wito katika kikao chao cha 35 wa kutaka makubaliano ya Septemba yabatilishwe na wapiganaji wa Ansarullah waondoke katika mji mkuu wa Yemen na katika maeneo mengine wanayoyadhibiti. Baadhi ya viongozi wa harakati ya Ansarullah akiwemo Ali al Bukhaiti, mjumbe wa baraza la kisiasa na Hussein al Azi, mkuu wa mahusiano ya nje katika ofisi ya kisiasa ya harakati hiyo wamepinga azimio au taarifa yoyote ya kuingilia masuala ya ndani ya Yemen na kusisitiza kwamba taarifa ya Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi ni ya uingiliaji, ni tusi kwa wananchi wa Yemen na ni njama ya kushadidisha hitilafu za kimatapo na kimadhehebu katika nchi hiyo…/

Wanajeshi 6 wa Afghanistan wauawa kwenye mlipuko

Basi lililokuwa limewabeba wanajeshi wa Afghanistan limeshambuliwa na mlipuaji wa kujitolea kufa viungani mwa mji mkuu, Kabul, ambapo wanajeshi 6 wameuawa na wengine 11 kujeruhiwa. Dawlat Waziri, afisa mwandamizi katika Wizara ya Ulinzi ya Afghanistan amesema mlipuaji huyo wa kujitolea kufa alikuwa akitembea kwa miguu wakati alipojilipua karibu na basi hilo leo mchana. Kundi la kigaidi la Taliban limedai kuhusika na shambulizi hilo na limesema wanajeshi waliouawa ni 12 na kwamba wengine 13 wamejeruhiwa. Kundi la Taliban pia limedai kuhusika na shambulizi jingine la leo asubuhi dhidi ya soko la umma katika mkoa wa Herat ulioko magharibi mwa Afghanisan. Serikali haijataja idadi ya waliouawa katika shambulizi hilo.
Katika wiki za hivi karibuni kundi la Taliban limeshadidisha mashambulizi dhidi ya majengo ya serikali, hoteli zinazotumiwa na raia wa kigeni pamoja na vituo vya polisi na jeshi ndani na nje ya mji wa Kabul.

Sudan iko tayari kukabiliana na makundi ya waasi

Mkuu wa Kitengo cha Intelijinsia nchini Sudan amesisitiza kuwa vikosi vya usalama vya nchi hiyo vimewekwa tayari kwa lengo la kukabiliana na vita vya pande zote dhidi ya makundi ya waasi nchini humo. Muhammad Atta al Mauli amesema kuwa, ulinzi na usalama unapaswa kuimarishwa zaidi kwa lengo la kukabiliana na makundi ya waasi yanayoleta chokochoko katika majimbo mbalimbali ya nchi hiyo. Al Mauli ameongeza kuwa, vikosi vya usalama vimejizatiti katika maeneo ya majimbo ya Kordofan Kusini na Darfur kwa lengo la kukabiliana na mashambulizi hayo ya waasi. Amesema kuwa, baadhi ya makundi yanajaribu kuwavunja moyo wananchi kwa kusambaza fikra na propaganda potovu kwamba jeshi la Sudan halina uwezo wa kupambana na makundi ya waasi. Inafaa kuashiria hapa kuwa, majimbo ya Kordofan Kusini na Darfur yanakabiliwa na machafuko kwa karibu miaka mitatu sasa, tokea Sudan Kusini ilipojitenga na Sudan na kuwa taifa huru.

Dafina ya Kanali Gaddafi yafichuliwa Afrika Kusini

Duru za habari kutoka Afrika Kusini zimetangaza kufichuliwa utajiri mkubwa na dafina iliyofichwa wakati wa kipindi cha utawala wa dikteta Muammar Gaddafi wa Libya nchini humo. Gazeti la Independent Online la nchini Afrika Kusini limeandika kuwa, zaidi ya dola bilioni 200, mamia ya tani za dhahabu, vipande milioni sita vya almasi na vito vya thamani vilitoroshwa na utawala wa Gaddafi na kuhamishiwa nchini Afrika Kusini. Taarifa zinasema kuwa, mali zote zilizotoroshwa na utawala wa dikteta Gaddafi nchini Afrika Kusini zimehifadhiwa kwenye maghala saba, na zinafikia zaidi ya dola trilioni mbili. Gazeti hilo limeandika kuwa, Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini na serikali yake wanakabiliwa na mashinikizo makubwa ya jamii ya kimataifa kuhusiana na mali na utajiri huo mkubwa wa wananchi wa Libya uliofichwa nchini humo. Imeelezwa kuwa, hivi sasa dafina hiyo iliyoibiwa kutoka Libya na kufichwa katika eneo la siri lililoko katika maeneo ya kati ya Johannesburg na Pretoria ilisafirishwa kwa kutumia zaidi ya shehena 62 za ndege kutoka Libya na kupelekwa Afrika Kusini mwishoni mwa utawala wa dikteta Gaddafi

Jonathan kuchuana na Buhari uchaguzi wa rais Nigeria

Uchaguzi wa urais nchini Nigeria unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa na wa aina yake baada ya vyama vikuu kuwachagua wagombea wao. Chama tawala cha PDP kimemteua Rais Goodluck Jonathan kuwa mgombea wake huku muungano mkuu wa upinzani wa APC ukimteua rais wa zamani, Jenerali Mohammadu Buhari kupeperusha bendera yake kwenye uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Februari 15 mwakani. Buhari amemshinda mpinzani wake wa karibu, Atiku Abubakar, ambaye ni makamu wa zamani wa rais wa nchi hiyo kwenye uchaguzi wa ndani wa APC uliofanyika hapo jana.
Kampeni za uchaguzi zinatarajiwa kuwa ngumu hasa kwa upande wa chama tawala kutokana na serikali kuonekana kushindwa kudhibiti kundi la kigaidi la Boko Haram. Pia serikali ya Rais Jonathan itakuwa na kibarua kigumu kuwashawishi wapiga kura kwani inatuhumiwa kuhusika na ufisadi. Wajuzi wa mambo wanasema Jenerali Buhari ana sifa nzuri ya kupambana na ufisadi kwani alipoingia madarakani 1983 kupitia mapinduzi ya kijeshi alichukua hatua muhimu kukabiliana na uozo huo kabla ya kuondolewa madarakani 1985 kwenye mapinduzi mengine ya kijeshi yaliyoongozwa na Ibrahim Babangida

Waziri wa Palestina aliyeuawa shahidi na Israel azikwa

Waziri wa serikali ya umoja wa kitaifa ya Palestina aliyeuawa shahidi kwa kupigwa hapo jana na mwanajeshi wa utawala haramu wa Israel amezikwa leo. Maelfu ya Wapalestina wakiongozwa na Rais Mahmoud Abbas wamehudhuria maziko ya Ziad Abu Ein huku waombolezaji wakimtaka Abbas achukue hatua kali dhidi ya utawala ghasibu wa Israel. Hapo jana madaktari walioupasua mwili wa Abu Ein kwa ajili ya kuchunguza chanzo cha kifo chake walisema kiongozi huyo alipoteza maisha baada ya kupata majeraha shingoni pamoja na kuvuta gesi yenye sumu. Utawala wa Kizayuni wa Israel umekataa kutambua ripoti ya madaktari licha ya kuwepo mwakilishi wake kwenye shughuli za upasuaji wa mwili wa Waziri Ziad. Utawala huo bandia umetoa taarifa ya upotoshaji na kusema Ziad Abu Ein alifariki dunia kutokana na mshituko wa moyo. Picha za video zinazoonyesha jinsi mwanajeshi mzayuni alivyomkaba koo waziri huyo wa Palestina zimesambaa katika mitandao ya kijamii na hivyo kuamsha hasira za ulimwengu kuhusiana na jinai hiyo ya Israel. Umoja wa Ulaya, Umoja wa Mataifa pamoja na nchi mbalimbali za dunia zikiwemo Iran na Russia zimelaani mauaji ya Waziri huyo na kutaka hatua kali zichukuliwe dhidi ya wale waliohusika na unyama huo.

Kenya yaimarisha usalama kukabiliana na al Shabab

Serikali ya Kenya imetangaza kuchukua hatua kali zaidi za kiusalama kwa lengo la kukabiliana na kundi la kigaidi la al Shabab la nchini Somalia. Taarifa kutoka Nairobi zinasema kuwa, hatua hiyo ya serikali ya Kenya imechukuliwa baada ya kushadidi mashambulio ya kundi la al Shabab nchini humo. Aidha serikali ya Kenya imeongeza muda wa kuwaweka rumande washukiwa wa ugaidi kutoka siku 90 hadi 360 pamoja na kusimamia kikamilifu idara ya mawasiliano nchini humo. Mpango huo pia umelenga kupunguza idadi ya wakimbizi wa kigeni walioko nchini humo na kufikia laki moja na nusu, ikilinganishwa na wakimbizi laki sita na elfu saba walioko hivi sasa kwenye kambi za wakimbizi nchini humo. Hali kadhalika, serikali ya Kenya imetangaza kuwa, waandishi wa habari ambao watapatwa na hatia ya kuzuia kufanyika uchunguzi na operesheni za kupambana na ugaidi watahukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela. Hali kadhalika, waandishi wa habari watakaotumia suhula za kijamii kwa lengo la kuwashawishi wananchi kutekeleza operesheni za kigaidi watahukumiwa adhabu ya kifungo cha miaka ishirini jela. Inafaa kuashiria hapa kuwa, serikali ya Kenya inakabiliwa na mashinikizo makubwa yanayotokana na mashambulio ya kigaidi, tokea kiliposhambuliwa kituo cha kibiashara cha Westgate jijini Nairobi mwezi Septemba mwaka jana, na kupelekea watu wasiopungua 67 kuuawa. Mapema mwezi huu, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya aliwafuta kazi Waziri wa Mambo ya Ndani pamoja na Mkuu wa Jeshi la Polisi baada ya kuongezeka mashambulio ya kundi la kigaidi la al Shabab katika maeneo ya kaskazini mashariki mwa nchi hiyo

Mauaji ya Waziri wa Palestina yachunguzwe haraka”

Mkuu mpya wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya amesisitiza juu ya udharura wa kufanyika uchunguzi wa haraka na huru kuhusiana na sababu ya kufa shahidi Ziad Abu Ein, Waziri Asiye na Wizara Maalumu wa Palestina. Federica Mogherini amebainisha kwamba, kuna haja ya kufanyika uchunguzi kuhusiana na sababu ya kifo cha waziri huyo. Aidha Mkuu wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya amesema kuna udharura kwa jamii ya kimataifa kuingilia kati kuhusiana na kile kinachojiri katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu. Wakati huo huo, Ban Ki-Moon Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa naye ameutaka utawala wa Kizayuni wa Israel ufanye uchunguzi kuhusiana na sababu ya kufa shahidi waziri huyo wa Palestina. Ikumbukwe kuwa, jana wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel walimuua shahidi Ziad Abu Ein, Waziri Asiye na Wizara Maalumu wa Palestina, kwenye vurugu zilizotokea kati ya askari wa Israel na wananchi wa Palestina katika kitongoji cha Turmus Ayya. Taarifa zinasema kuwa, wanajeshi wa Israel walianza kuwafyatulia gesi ya kutoa machozi Wapalestina waliokuwa wakipanda mizaituni kulalamikia ujenzi wa ukuta wa kidhalimu wa Israel katika eneo la Turmus Ayya lililoko kaskazini mwa Ramallah. Ziad Abu Ein ambaye alikuwemo kwenye maandamano ya Wapalestina ya kupinga ujenzi wa ukuta huo alipigwa na kitu kizito kichwani na kupoteza fahamu, na juhudi za kuokoa maisha yake zilishindikana kutokana na kuzidiwa na gesi.

Thursday, 11 December 2014

VIJANA WA FORODHANI WAKIWA KATIKA MAZOEZI KUJITAYARISHA NA PAMBANO KUU


VIJANA WA FORODHANI MJINI ZANZIBAR WAKIWA KATIKA MAZOEZI YA KUJI TAYARISHA NA PAMBANO LA SIKU YA JUMAAMOSI YA TAREHE 13/12/2014 HAPO FORODHANI PARK MNAKARIBISHWA