Unordered List


Blogger Tips and TricksLatest Tips And TricksBlogger Tricks

Tuesday, 25 November 2014

Serikali imewekeza katika siasa, imesahau wakulima

Serikali imewekeza katika siasa, imesahau wakulima

 
Hata hivyo, wakulima wamekwazwa na kodi nyingi wanazotozwa kwa kila gunia inapotokea wakauza sehemu ya mahindi yao yaliyolundikana. Malipo hayo ni kama kodi ya halmashauri, gharama za kuhifadhi mahindi ghalani, ubebaji wakati wa kushusha mahindi kituoni, kuchekecha mahindi, kuondoa uchafu na kupeleka kwenye mizani. 
Kwa ufupi
Siyo siri kuwa, iwapo fedha inazotumia katika mambo ya kisiasa zingeelekezwa kwenye kilimo, wakulima wangejikomboa kiuchumi.
Zipo dalili nyingi zinazoonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa nchi yetu ikakumbwa na janga kubwa la njaa mwakani. Kinachoendelea hivi sasa ni wakulima katika mikoa inayolima mazao ya chakula kwa wingi kukata tamaa kutokana na mazao yao kukosa soko, huku wakulima hao wakijikuta katika ufukara wa kutisha kutokana na kuwekeza fedha zao katika kilimo cha mazao hayo, lakini Serikali imeshindwa kuwatafutia masoko.
Hapa hatuzungumzii mazao ya biashara kama korosho, tumbaku, kahawa na pamba ambayo kwa muda mrefu sasa yamegeuka kuwa laana kwa wakulima kutokana na viongozi wa vyama vya ushirika nchi nzima kuvigeuza vyama hivyo kama mitaji binafsi ya kujitajirisha wakishirikiana na baadhi ya viongozi serikalini.
Kwa miongo minne sasa wakulima hao hawana sauti wala mtetezi. Serikali ingetarajiwa kuvikwamua vyama hivyo, ambavyo vilianzishwa na wakulima wenyewe na kuwa nguzo yao kubwa kiuchumi. Hata hivyo, hakuna asiyejua kwamba Serikali kwa kuogopa nguvu ya vyama hivyo, iliingilia kati na kuvisambaratisha kwa kupandikiza uongozi uliowekwa mfukoni na wanasiasa.
Hapa tunazungumzia wakulima wa mazao ya chakula, hasa mahindi yanayolimwa kwa wingi katika mikoa ya Mbeya, Rukwa, Katavi, Ruvuma, Iringa na Morogoro inayojulikana kama ‘Kapu la Chakula’. Hivi sasa wakulima wa zao hilo wamekata tamaa kutokana na kukosa soko la zao hilo, hivyo hawaoni tena sababu ya kuwekeza katika kilimo hicho kutokana na hasara waliyoipata msimu uliopita, ambao walikopa fedha kuandaa mashamba na kununua pembejeo na kufanikiwa kuvuna kiasi kikubwa cha mahindi. Wakulima walihamasika kutokana na Rais Jakaya Kikwete kutangaza bei mpya ya mahindi kutoka Sh350 hadi Sh500 alipokuwa katika ziara ya mkoani Ruvuma mwaka uliopita.
Matokeo yake ni kwamba mahindi yanaozea katika makazi ya watu, maghala ya vyama vya ushirika, Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NRFA) na wafanyabiashara binafsi. Wakulima wamebaki wakiwa midomo wazi, wakisubiri kuona miujiza ya mahindi yao kupata soko ili wajikwamue katika ufukara na umaskini uliopitiliza. Takwimu zinaonyesha kwamba mikoa hiyo imezalisha tani milioni 16 za mahindi, huku Mkoa wa Rukwa pekee ukizalisha tani milioni nne.
Hata hivyo, wakulima wamekwazwa na kodi nyingi wanazotozwa kwa kila gunia inapotokea wakauza sehemu ya mahindi yao yaliyolundikana. Malipo hayo ni kama kodi ya halmashauri, gharama za kuhifadhi mahindi ghalani, ubebaji wakati wa kushusha mahindi kituoni, kuchekecha mahindi, kuondoa uchafu na kupeleka kwenye mizani.
Kutokana na umuhimu wa sekta ya kilimo ambayo inatoa ajira kwa zaidi ya asilimia 80 ya wananchi, tungetarajia Serikali iwekeze nguvu na rasilimali zake kwenye kilimo. Mipango ya Kilimo Kwanza na Matokeo Makubwa Sasa imeonekana kuwa ni nadharia zaidi kuliko utekelezaji. Ni kutokana na hali hiyo tunaishauri Serikali iwekeze kwa wakulima badala ya kuwekeza kwenye siasa. Siyo siri kuwa, iwapo fedha inazotumia katika mambo ya kisiasa zingeelekezwa kwenye kilimo, wakulima wangejikomboa kiuchumi.
Ni wakati wa Serikali sasa kufikiri nje ya kisanduku kwa kuwatafutia wakulima masoko ya uhakika kwa mazao yao, yakiwamo matunda kama nyanya, maembe, machungwa na nanasi yanayoozea mashambani kwa kukosa viwanda vya kusindika. Kipaumbele kiwekwe kwa wakulima na Serikali itambue kwamba wananchi hawawezi kupata shibe kutokana na siasa.

No comments:

Post a Comment